0
SIMBA ilikwenda Zanzibar kushiriki michuano ya Kombe la Mapinduzi ikiwa na kikosi kilichokuwa hakipewi nafasi kubwa ya kufika mbali.


Timu kama mabingwa watetezi, KCC ya Uganda, Azam FC na Yanga, walionekana kuwa na nafasi ya kusonga mbele.

Hata kundi lao la B lilibatizwa jina la “kundi la kifo”, Simba ilikuwa Kundi C ambalo lilionekana halina lolote, kwamba ni laini.

Wakati kesho fainali ya Kombe la Mapinduzi inapigwa kwenye Uwanja wa Amaan, Zanzibar timu zilizotinga fainali zote ni kutoka Kundi C, Mtibwa Sugar na Simba.

Simba inakutana na Mtibwa Sugar iliyoanza michuano hiyo kwa kuifunga bao 1-0 katika mechi ya kwanza ya Kundi C.

Wakati Simba inalala bao 1-0 dhidi ya Mtibwa Sugar ilikuwa chini ya Kocha Msaidizi, Selemani Matola lakini ikaonyesha uwezo mkubwa.

Sasa Simba imeongeza nguvu, Matola atakuwa akimsaidia Goran Kopunovic kuhakikisha Simba inabeba ubingwa wa Kombe la Mapinduzi.
 Kocha huyo mpya wa Simba raia wa Serbia, anaamini kikosi chake kinaweza kubeba ubingwa huo lakini anasisitiza anachoendelea kuangalia ni mabadiliko katika kikosi chake.

Ndani ya siku chache, uchezaji wa Simba sasa umekuwa zaidi katika mfumo wa tiki-taka ambao hutumiwa zaidi na timu za Hispania hasa Barcelona na ile timu ya taifa hilo.

Tiki-taka ni aina ya uchezaji wa pasi fupifupi huku timu ikitembea kutoka sehemu moja kwenda nyingine kwa haraka, hali kadhalika hufanya hivyo wakati wa ukabaji inaposhambuliwa.

Kopunovic anakiri michuano hiyo ni muhimu kwa maana ya hadhi na kuongeza ari kwa kikosi chake lakini yeye na msaidizi wake, Matola wanaitumia vizuri kukijenga kikosi chao upya kabla ya kurejea Ligi Kuu Bara.

Katika mahojiano mafupi na gazeti hili, Kopunovic anasema kumekuwa na mambo ya kubadilisha.

Kwanza anaanza na kumshukuru msaidizi wake, Matola kwamba ameonyesha ushirikiano mkubwa, pia ni mtu anayejituma.

“Naweza kusema kocha anakuwa hana ugeni, lakini unahitaji kupata watu sahihi wa kufanya nao kazi, hilo nashukuru.

“Matola anajituma na tunashirikiana vizuri, wachezaji wananisikiliza na wanaendelea kubadilika. Katika soka, mabadiliko ni jambo la kila siku.

“Ukibadilika leo, kesho unakutana na timu inacheza tofauti, unalazimika kubadilika tena,” anasema.

Aina ya soka:
Soka la kisasa ni kucheza pamoja wakati wa kushambulia na kufanya hivyo wakati wa kulinda.

Umesema tik taka, naweza kusema ndiyo, ingawa sipendi kuzungumzia uchezaji wa timu nyingine kama Barcelona au Bayern Munich kwa kuwa kila kocha ana falsafa yake ya ufundishaji.

Lakini tunakimbia wote kwenda mbele na kurudi pamoja. Huu si mfumo rahisi, si kila mchezaji atauweza ndani ya siku chache, ila tunapambana vilivyo kuhakikisha unawezekana.

Vipaji:
Simba ina vipaji vingi sana, hata kama utaangalia harakaharaka utaliona hilo. Hivyo si rahisi kubadilisha kila kitu mara moja, muda unahitajika.

Kweli niliwahi kumbadili mshambuliaji Meddy Kagere wa Polisi Rwanda na kuwa tishio, hilo pia linawezekana kwa Simba.

Bado niseme nitaendelea kuangalia vipaji, kutokana na nitakavyoona, ndivyo ninaweza kuwabadilisha baadhi ya wachezaji na kuzidi kuwa bora zaidi.

Kocha pia ana kazi ya kuwabadili wachezaji wake kwa maana ya kuwaongezea ubora walionao sasa upande zaidi.

Nidhamu:
Huu ni msingi, kama hakuna nidhamu hakuna mafanikio. Nidhamu ya kila sehemu, hadi uwanjani na ndiyo mambo yanaweza kwenda sahihi.

Tunaendelea kurekebishana, kitu kizuri ni kwamba tunashirikiana vizuri. Matumaini yangu tutafanikiwa baada ya muda na kuwa timu inayoelewana na kuaminiana.

Nafasi:
Kweli hatuzitumii vizuri nafasi tunazozipata. Taratibu tunafundishana na kutaka kuwe na mabadiliko katika hili. Kukiwa na nafasi, basi zitumike ili kuleta manufaa kwenye kikosi.

Pasi:
Kweli, pasi nyingi ni jambo zuri. Utaona katika mechi dhidi ya JKU, tumecheza hivyo lakini bado si kwa kiwango nilichotaka.

Kama nilivyosema mwanzo, tunashirikiana na Matola na wenzangu wa benchi la ufundi kuendelea kuleta mabadiliko.

Pasi nyingi zina faida yake kwa kuwa mnakuwa na mpira na pili mnapanga mnachotaka kufanya wakati mpira mnao, hamuwezi kufanya hivyo kama hamna mpira.

Mtibwa Sugar:
Nimeiona wakati inacheza baadhi ya mechi za Kombe la Mapinduzi, ni timu nzuri lakini ninachoweza kukuhakikishia itakuwa ni mechi ngumu.

Siku mbili tulizonazo tunaweza kubadilisha mambo kadhaa na kuangalia nini kizuri cha kufanya katika mechi hiyo inayokuja na ikiwezekana tubebe ubingwa.

Post a Comment

AddThis

 
Top