0
KAULI ya Roberto Mancini kuhusiana na mchezaji wake wa zamani, Mario Balotelli inaweza kuwa dawa au sumu kwa mshambuliaji huyo.


Mancini raia wa Italia ambaye amekuwa kimya muda mrefu ameibuka na kusema, Balotelli anapaswa kutambua Liverpool itakuwa nafasi yake ya mwisho.
 
Kocha huyo aliyeipa Man City ubingwa wa England baada ya zaidi ya miaka 40 akiwa na Balotelli, amesema ni wakati wa Balotelli kuonyesha alichonacho, la sivyo ataanza kuporomoka kwa kasi.
 
Mwendo wa Balotelli tokea atue Liverpool umekuwa ni wa kusua, tofauti na wengi walivyokuwa wakitegemea kutokana na uwezo wa kucheza alionao.
Mambo yamekuwa tofauti, ugumu wa mambo umeongezeka na tayari ile presha ya Kingereza imeanza juu yake.
Hoja kubwa kwa kuwa hajafunga mabao, bora Liverpool ingemtumia Rickie Lambert ambaye licha ya kutokea benchi amekuwa akifanya vizuri zaidi.
 
Achana na hivyo, Waingereza wana uwezo mkubwa wa kutengeneza presha, wamemhamishia Balotelli hadi kwenye suala la bei, kwamba alinunuliwa kwa pauni milioni 16 kutoka AC Milan sawa na zile alizonunuliwa Danny Welbeck akitua Arsenal kutoka Man United.
 
Wanasema Welbeck amekuwa akifunga mabao, tayari ameonekana atakuwa hatari zaidi. Lakini Balotelli bado anasua na vituko ndiyo vinachukua nafasi.
 
Kwenye mkataba wake na Liverpool, amebanwa mambo mengi sana hasa kuhusiana na nidhamu. Inaonekana kulikuwa na mjadala mkubwa kabla ya kufikia uamuzi wa kumsajili.
 
Lakini hakuna aliyeonyesha hofu kwake kutokana na uwezo wake na hata upachikaji mabao. Lakini tokea ametua Liverpool, kikubwa alichoonyesha ni uwezo mkubwa wa mashuti yaliyolenga bao akiwa sawa sasa na Diego Costa ambaye anaongoza kwa mabao.
 
Balotelli anajulikana kwa uwezo mkubwa wa kupuuza, uwezo wa juu wa kuendelea na anachotaka bila ya kujali. Lakini si mgeni wa presha za Kingereza.
 
Kikubwa lazima afunge, hilo halina mjadala kwa kuwa kila mmoja kwa mashabiki wa Liverpool kuanzia Tanzania, England na kwingineko wanataka kumuona anafunga, hakuna mjadala.
 
Hadi sasa kinachoonekana ni kuwa takwimu zinambana, hata ukiangalia wakati akiwa Inter Milan, Man City na AC Milan, alikuwa na vitu vizuri zaidi ‘alivyotoa’.
 
Lakini tokea ametua Liverpool, bado haijakaa vizuri kwake na hana ujanja, achague kufunga au kukubaliana na Mancini ambaye walikuwa wakikwaruzana mara kwa mara kuwa ataporomoja haraka na ndiyo utakuwa mwisho wake.
TAKWIMU:
INTER MILAN:
Mechi      59
Kaanza   35
Dakika    3315
Mabao     20
Kuotea    26
MAN CITY:
Mechi      54
Kaanza   33
Dakika    3000
Mabao     20
Kuotea    25
AC MILAN:
Mechi      43
Kaanza   37
Dakika    3438
Mabao     26
Kuotea    23

Post a Comment

AddThis

 
Top